Pages

Monday 1 October 2012

YANGA YABEBWA NA KIUNGO NIZAR!!


Kiungo Nizar Khalfani alifunga mara mbili na beki Nadir Haroub 'Cannavaro' akaongeza jingine moja wakati Yanga iliposhinda 3-1 mbele ya kocha wao mpya Mholanzi Ernie Brandts aliyekuwa jukwaani na kuipa African Lyon kipigo cha tatu katika mechi nne za ligi kuu ya Bara kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam jana.

Nizar aliyeingia katika dakika ya 61 kuchukua nafasi ya Frank Domayo, alihitaji dakika 2 kuandika goli lake la kwanza na la pili kwa timu yake katika dakika ya 63 akiunganisha kwa kichwa krosi ya Simon Msuva na akaifungia Yanga la tatu katika dakika ya 88 akiuwahi mpira wa 'tik-taka' ya Said Bahanunzi iliyogonga 'besela' na kuangukia mbele ya lango.

Yanga ndio walitangulia kwa goli la mapema dakika ya 16 kupitia kwa beki wa kati Cannavaro aliyepanda mbele kusaidia mashambulizi na kufunga kirahisi kwa pasi ya kupenyezewa huku mabeki wakidhani ameotea, matokeo yaliyodumu hadi wakati wa mapumziko.

Licha ya kutawala mechi kwa muda mwingi kufikia kukaa na mpira kwa asilimia 65 dhidi ya 35 za Lyon, Yanga walipigwa goli la shambulizi la kustukiza katika dakika ya 62 kupitia kwa Benedictor Mwamlangala kufuatia pasi tamu ya Jacob Masawe.

Sherehe kubwa za "kupita kipimo" za kushangilia goli hilo zilizoonekana hata kwa kocha wao Muargentina Baplo Ignasio Velez aliyeonekana "kupagawa" kwa kusawazisha, zilionekana kuwagharimu Lyon, ambao walijikuta wakifungwa goli la pili kwa shambulizi la moja kwa moja kutokea kwenye 'kisanduku' cha kuanzia mpira cha katikati ya uwanja.

Pasi ndefu ya kuelekea kwenye wingi ya kushoto ilimkuta Msuva alimyemimina krosi katikati iliyotua kichwani mwa Nizar aliyefunga goli lake la kwanza kwenye ligi kuu tangu aliporejea nchini akitokea Marekani alikokuwa akicheza soka la kulipwa kabla ya kuongeza lake la pili dakika mbili kabla ya firimbi ya mwisho.

Kocha wa muda, Fred Minziro, aliyeiongoza Yanga katika mechi mbili alizoshinda zote tangu kufukuzwa kwa kocha wao Mbelgiji Tom Saintfiet, alisema baada ya mechi hiyo kwamba licha ya ushindi, timu yake ilipoteza nafasi nyingi za kufunga na ingeweza kupata matokeo mazuri zaidi ya hayo.

Alisema akili zao sasa wameziweka katika mechi kubwa ya Jumatano dhidi ya mahasimu wao Simba na kwamba wachezaji wake watarejea wakiwa wapya zaidi kiufundi. 

Katika mechi iliyopita baina ya timu hizo zenye upinzani wa jadi, Yanga ilikumbana na kipigo cha aibu cha 5-0.

Vikosi vilikuwa; Yanga: Ali Mustapha 'Barthez', Mbuyu Twite, Oscar Joshua/ Stephano Mwasika (dk.88), Kelvin Yondani, Nadir Haroub 'Cannavaro', Athuman Idd 'Chuji', Frank Domayo/ Nizar Khalfan (dk. 61), Frank Domayo, Didier Kavumbagu, Hamis Kiiza/ Said Bahanunzi (dk.58) na Haruna Niyonzima. 

African Lyon:
Abdul Seif, Omar Mtaki, Hamad Manzi, Sunday Bakari/ Idd Mbaga (dk.78), Benedictor Mwamlangala/ Fred Lewis (65), Robert Mkotya/ Semmy Kessy (dk. 50), Obina Salamusasa, Mohamed Samata, Hood Mayanja, Jacob Masawe na Yusuf Mlip

0 comments:

Post a Comment